Wataalamu wa Teknolojia ya mawasiliano wakutana kujadili kuundwa kwa mfumo wa pamoja wa kidigitali utakaowezesha Mifumo ya Serikali na binafsi kubadilishana taarifa (Digital ID Ecosytem for Tanzania)

Wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano nchini wanakutana katika warsha ya Siku mbili mkoani Pwani kujadili namna ya kutengeneza mfumo wa Taifa wa Kidigitali utakaowezesha mifumo ya Serikali na Binafsi kubadilishana taarifa kwa kutumia Mfumo Mkuu wa Taifa wa Usajili na Utambuzi wa Watu unaosimamiwa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa(NIDA).

Warsha hiyo iliyoandaliwa kwa pamoja na World Bank na NIDA imefunguliwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Balozi Hassan Yahya Simba ambaye amepongeza hatua hii muhimu kwa Taifa ya kuwa na mfumo utakaowezesha kuunganisha mifumo ya Serikali na Binafsi katika masuala ya Utambuzi kwa manufaa mapana ya Taifa.

Amesema kuwepo kwa mfumo imara wa Utambuzi kutawezesha sio tu maendeleo ya haraka ya Taifa, lakini pia kutaruhusu wananchi kupata haki zao kwa wakati na kuboresha huduma za kijamii; na kusaidia Serikali na sekta binafsi kuwafikia wananchi kirahisi  na kutoa huduma zenye viwango.

Akizungumza kwa niaba ya Benki ya Dunia (World Bank) ambao wamefadhili warsha hiyo, ndugu  Robert Palacios amesema Benki ya Dunia kwa kutambua umuhimu wa Serikali kutoa huduma bora kwa wananchi na kwa kutambua changamoto kubwa ya idadi kubwa ya wananchi kutotambulika na mifumo rasmi kwa kukosa mfumo rasmi unaowatambua, Benki ya Dunia imeamua kusaidia harakati za nchi za Afrika katika kukamilisha kuanzishwa kwa mfumo wa Utambuzi na kuunganishwa kwa mifumo ya utoaji huduma ili kuwezesha wananchi kupata huduma kwa haraka na kuinua hali za maisha hususani wananchi wanaoshi katika hali ngumu.

Warsha ya Wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano imeanza leo (18 – 19/09/2017) Bagamoyo mkoani Pwani katika hoteli ya Ocenic Bay na inatazamiwa kuibuka na maazimio yatakayoiwezesha Serikali kuwa na Sera na mikakati ya pamoja katika kuunda mfumo wa kidigitali wa matumizi ya Taarifa kwa Serikali na wadau katika utoaji huduma. Miongoni mwa washiriki katika warsha hiyo ni Wizara, Mashirika,  Taasisi na Makampuni binafsi.

Ndugu Jonathan Marskell wa Benki ya Dunia (World Bank) akizungumza kutambulisha wageni walioshiriki katika warsha ya wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano.

 

Mhe. Balozi Hassan Yahya Simba akifungua warsa ya wataalamu wa wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano Bagamoyo.

 

Baadhi ya Washiriki wa Warsha ya Wataalamu wa Teknolojia ya Mawasiliano wakifuatilia mada zilizowasilishwa. Kulia ni ndugu Gideon Ndalu Mkurugenzi Mifumo ya Komputa na Ndugu Solanus Mhenga Kaimu Mkurugenzi Idara ya Sheria NIDA.

 

Wa kwanza kushoto ni ndugu Vijay Madan, Mkurugenzi Mkuu wa zamani Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa India, Katikati ni  ndugu Margus Puua, Mtaalamu kutoka chuo cha mafunzo Serikali Huduma Mtandao Estonia na pembeni ni Dr. Elias Mturi wa Chuo Kikuu cha Dar-es-salaam Idara ya Komputa ambaye ndiye mwezeshaji katika mkutano huo.

 

Mhe. Balozi Hassan Yahya Simba (Katikati) akifuatilia kwa makini mjadala unaondelea kuhusu kuundwa kwa mfumo wa kidigitali unaohusu matumizi ya taarifa. Kulia ni ndugu  Robert Palacios mwakilishi wa Benki ya Dunia na Kushoto ni ndugu Alphonce Malibiche akimwakilisha Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa Ndugu Andrew W. Massawe.

 

Washiriki wa Warsha ya Teknolojia ya Mawasiliano Bagamoyo wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni Rasmi Mhe. Balozi Hassan Yahya Simba baada ya ufunguzi wa Rarsha.

 

 

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Taarifa Kwa Umma

Ukurasa wetu wa Facebook

Ramani ya Ofisi Zetu